Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Kibondo, Alex Sylvester Baragomwa amechaguliwa kuwa Mwenyekiti mpya wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania Mkoa wa Kigoma (ALAT) na kuwasisitiza wenyeviti wa Halmashauri kwenda kushirikiana ipasavyo na Wakurugenzi watendaji katika kukusanya mapato.
Akitangaza matokeo ya ushindi huo, Katibu wa kikao, Ndaki Stephano Mhuli amemtangaza Mhe.Alex Baragomwa kuibuka na ushindi wa nafasi ya mwenyekiti wa halmashauri baada ya kuwashinda wagombea wenzake watatu kwa kupata kura 12 kati ya wajumbe 30 walioshiriki zoezi la kupiga kura.
Mwenyekiti aliyechaguliwa, Alex Baragomwa amewashukuru wajumbe kwa kumchagua na kueleza kuwa analenga kutengeneza mahusiano baina ya Madiwani na Halmashauri ili kuwa na umoja wa pamoja kama Mkoa.
“Sisi wenyeviti wa Halmashauri ndio watu ambao tunaweza tukatoa mtazamao wa maendeleo katika halmashauri zetu kwa hiyo niwaombe sana wenyeviti wa halmashauri wenzangu twende tukashirikiane vyema katika kukusanya mapato ya halmashauri”, alieleza Mhe.Baragomwa.
Aidha katika kikao hicho, Mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Kasulu, Mhe.Ayubu Ngalaba alipita bila kupingwa katika nafasi ya makamu mwenyekiti baada ya kuwa mgombea pekee katika nafasi hiyo.
Kikao hicho kilichohusisha Wenyeviti wa Halmashauri za Mkoa wa Kigoma, Wakurugenzi watendaji na waheshimiwa madiwani wawili kwa kila halmashauri ambao ni wajumbe wa ALAT Mkoa kimefanyika leo Alhamisi 29 Januari, 2026 Wilayani Kakonko katika ukumbi mpya wa Halmashauri uliopo eneo la Kanyamfisi ambapo zipo ofisi za halmashauri.
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko
Anuani ya Posta: P.O.BOX 3
Simu: +255(028) 2988881
Simu ya Mkononi: +255(028) 2988881
Barua Pepe: ded@kakonkodc.go.tz
Hatimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko. Haki zote zimehifadhiwa