Watumishi wa Halmashauri Wilayani Kakonko wamesisitizwa kuzingatia maadili ya utumishi wa Umma na kuimarisha utendaji wao wa kazi kupitia mifumo ya usimamizi wa utendaji (PEPMIS).
Wito huo umetolewa na Afisa Habari mkuu kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala bora, Rocky Robert Setengo wakati akitoa mafunzo ya kanuni za maadili ya utendaji katika utumishi wa umma kwa watumishi Wilayani Kakonko.
Mafunzo hayo yamelenga kufanya uhamasishaji wa maadili kwa watumishi wa umma kwa kuwakumbusha na kujengeana uelewa katika masuala ya usimamizi wa maadili pamoja na utekelezaji wa majukumu katika maeneo yao ya kazi.
“Watumishi wa umma tunawasisitiza kuhakikisha kwamba wanaheshimu kanuni 8 za maadili ya utendaji katika utumishi wa umma pamoja na kuzisimamia ipasavyo,”, ameeleza Setengo.
Aidha amewataka watumishi wanapokuwa wanatoa huduma wazingatie kanuni zote 8 pamoja na waraka wa mavazi kwa watumishi wa umma kuepuka malalamiko ya Wananchi juu ya ucheleweshwaji wa huduma, lugha isiyo ya staa, uvaaji usio mzuri, na kutofika ofisini kwa wakati.
Akifafanua kile kilichofundishwa afisa utumishi, Fabius Jeremiah ameeleza kuwa wamejifunza kanuni 8 ikiwemo kufanya kazi kwa bidii, kuheshimu sheria na kutoa huduma bila upendeleo hivyo ameahidi kwa niaba ya watumishi kuhakikisha yale yote waliyoelekezwa wanakwenda kufanyia kazi.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo, Anderson Salum silvestor, Mtendaji wa Kata ya Kiziguzigu ametoa shukrani kwa mafunzo waliyopata kuhusiana na maadili katika utumishi wa umma.
“Kimsingi maadili ya utunmishi wa umma yanabeba taswira nzima ya uwajibikaji wa serikali kwa watu wake, kwa hiyo sisi kama watumishi wa umma tunao wajibu wa kuhakikisha kwamba tunatekeleza na kuzingatia maadili ya umma ili kuisaidia serikali yetu na viongozi wetu katika kuwajibika kwa watu wake”, alieleza Anderson.
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala bora kupitia Idara ya usimamizi wa maadili imetoa mafunzo hayo kwa Wakuu wa Idara na Vitengo wa Halmashauri pamoja na Watumishi wa Halmashauri siku ya Jumatatu tarehe 19 Januari, 2026 katika Ofisi za Halmashauri pamoja na Ukumbi wa Halmashauri uliopo Wilayani Kakonko.
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko
Anuani ya Posta: P.O.BOX 3
Simu: +255(028) 2988881
Simu ya Mkononi: +255(028) 2988881
Barua Pepe: ded@kakonkodc.go.tz
Hatimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko. Haki zote zimehifadhiwa