Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Bi. Aviana Philipo ambae ni Afisa Tarafa Kata ya Nyaronga akimwakilisha Mkuu wa Wilaya Kanali Evance Mesha Mallasa amewahimiza vijana kuzingatia kilimo kwani kilimo ndio mkombozi wa familia na huongeza kipato.
Bi.Aviana amewasisitiza vijana mara baada ya kupatiwa mafunzo wakawe mfano katika jamii kwa kulima mazao mengi hasa mahindi lishe na maharage lishe na kutoa elimu kwa wakulima katika jamii inayowazunguka.
Amesema hayo leo Septemba 21,2023, wakati alikifungua mafunzo ya kilimo kwa vijana ambayo yamefanyika katika ofisi ya kata Kiziguzigu na yamewahusisha vijana kutoka Kata ya Kanyonza na Kiziguzigu.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko Ndugu Revocatus Nandi ambae ni Afisa Kilimo akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji Ndugu Ndaki Stephano Mhuli amewaasa Vijana kuwekeza katika kilimo kwa kufuata njia bora za kilimo wanazoelekezwa na wataalam na kuepuka kuwa tegemezi kwa wazazi.
Aidha Ndugu Nandi amewasisitiza vijana kutumia mbegu bora na kutumia mbolea za kupandia, kukuzia na kubebeshea mimea ili kuongeza uzalishaji wa mazao. Pia amewataka vijana wote kuwa na shamba la mfano na si kutegemea shamba darasa na wakawe wawezeshaji kwa wakulima wengine.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Kiziguzigu Mhe. Martin Mpemba amewataka vijana kujikita katika kilimo kwani hata Serikali inasisitiza Vijana kujiajiri kupitia kilimo na kuepuka kutegemea kuajiriwa na inaendelea kuwainua vijana katika kilimo kupitia programme ya (BBT) Build Better Tommorow.
Baraka Joshua mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka Shirika la Nyakitonto Youth Development in Tanzania ameeleza lengo la Shirika ni kutoa elimu kwa vijana juu ya mbinu bora za kilimo na kuwahimiza vijana kujikita katika kilimo cha kisasa chenye tija kwa kupanda mbegu ambazo zimethibitishwa na wataalam kwa kuzingatia vipimo sahihi wakati wa kulima na kupanda mbegu.
Aidha ameeleza katika mafunzo hayo vijana wamefundishwa umuhimu na faida ya kulima mazao lishe pia wataelekezwa kwa vitendo namna ya kulima mazao lishe kupitia shamba darasa ambapo watajikita katika uzalishaji wa mahindi lishe na maharage lishe.
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko
Anuani ya Posta: P.O.BOX 3
Simu: +255(028) 2988881
Simu ya Mkononi: +255(028) 2988881
Barua Pepe: ded@kakonkodc.go.tz
Hatimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko. Haki zote zimehifadhiwa